Monday, April 1, 2019

2⃣5⃣ MAMBO MUHIMU UNAYOTAKIWA UYAFANYE ILI UPATE KUISHINDA DHAMBI YA UZINZI

2⃣5⃣ MAMBO MUHIMU UNAYOTAKIWA UYAFANYE ILI UPATE KUISHINDA DHAMBI YA UZINZI

Na: MWL STEVEN & BETH MWAKATWILA

KUPATA APP YETU “HUSONEMU (MWAKATWILA) APP” BONYEZA LINK HII HAPA:

FUATANA NASI:- KWENYE APP, FACEBOOK, INSTAGRAM, ONLINE RADIO 📻, WHATSAPP, WEBSITE & YOUTUBE, Kwa links zilizoko kwenye HII LINK hapa:

🗓 01 Aprili, 2019

Bwana Yesu Kristo asifiwe sana. Ninamshukuru Mungu sana kwa mambo mema mno anayotutendea. Nimekuletea somo. Somo hili litakuwa linatufikisha mwisho wa mfululizo mzima wa somo hili.

Naamini kuna kitu kwa sehemu umejifunza, nakushauri yaweke  kwenye matendo yale uliyojifunza. Yatakusaidia kuishinda dhambi ya uzinzi. Usisite kuniuliza swali mahali haujaelewa au unapohitaji msaada wa kishauri au hata maombi.

Hebu sasa tuendelee mbele. Nilianza kukuonyesha milango ambayo inayoweza kuwa chanzo cha pepo kumrudia mtu. Baada ya kukuonyesha mfumo wa dhambi  unavyoweza kumpatia adui uhalali nataka nikuonyeshe kwa upana zaidi eneo hili la dhambi.
Bwana Yesu Kristo anatufundisha kuwa pepo mchafu amtokapo mtu ana tabia ya kufanya majaribio ya kumrudia tena huyo mtu. Maandiko yanatufundisha hivi.

“Pepo mchafu amtokapo mtu, hupitia mahali pasipo maji, akitafuta mahali pa kupumzika; asipoona, husema, Nitairudia nyumba yangu niliyotoka. Hata afikapo, akaiona imefagiwa na kupambwa, ndipo huenda akachukua pepo wengine saba, walio waovu kuliko yeye mwenyewe, wakaingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza.” (Luka11:24-26).

Ukiipitia hiyo mistari utagundua kuwa pepo lolote lile linapotolewa ndani ya mtu hapo Bwana ameita nyumba linakuwa na tabia ya kutafuta mpenyo wa kuirudia hiyo nyumba au kumrudia huyo mtu.

Kinachosababisha hamu au shauku ya kurudi ni mazingira ya hiyo nyuma au huyo mtu. Kuna vitu ataviona kwa huyo mtu navyo ni mfumo wa kumvutia. Mapepo yanavutiwa na dhambi zisizofubiwa. Hapo namaanisha hivi, unaweza kutenda dhambi lakini unaificha badala ya kuiungama na kuiacha.

Watu wengi waliotolewa mapepo hawajui kuwa wanapohifadhi dhambi au kuitenda hiyo dhambi mara kwa mara wanajiletea hatari ya kurudiwa na mapepo tena yanarudi mengi kuliko yale ya kwanza.

Nakumbuka niliwahi kukutana na binti mmoja ambaye alikuwa anafuatiliwa na shetani. Alinisimulia habari ndefu sana, alikuwa na mikataba na shetani na akamtumikia sana tu.
Baadaye akakutana na Bwana Yesu Kristo mapepo yaliyokuwa ndani yake yakatolewa akawa huru. Baada ya muda akashangaa anamwona shetani akimfuata na kudai anataka wafunge tena agano ili aendelee kumtumikia, wakati ananisimulia habari hiyo.

Niligundua moyoni mwangu kuwa lazima kutakuwa na mlango ambao shetani anautumia ili kumrudia huyo binti ingawa huyo binti hataki. Nilijua kuwa kuna kitu kibaya tu afanyacho huyo binti kinachomba shetani mvuto tena wa kumfuatilia huyo binti.

Nikamwuliza je! Ana mahusiano yoyote na kijana wa kiume? Akasema ndiyo. Nikamkazia macho niambie mahusiano yenu yakoje? Unajua niligundua katika mahusiano yao na huyo kijana wamevuka mpaka mnoo.  Wanaweza kukumbatiana kutomasana mpaka kupigana busu ya kikubwa!!!! wengine wanaita busu la ulimi. Nikamwambia dhambi hiyo ndiyo mlango wa shetani anautumia ili kukurudia.

Akaniambia itakuwa ni kweli kwani tokea ameanza mahusiano na huyo kijana tu ndipo anamuona shetani akianza kumfuatilia. Yeye alikuwa anayaona mapepo macho kwa macho kwani alikuwa na mambo ya ajabu kweli huyo binti. Kufunguliwa kwake tu ilikuwa si mchezo.

Nikamwamuru aachane na huyo kijana haraka sana kwa usalama wake. Alinikubalia.  Sasa sikia, unapotolewa mapepo fahamu tena kuwa adui atataka kurudi na atatumia mfumo wa tabia zako mbaya ili kuwa mlango wa kuingilia tena ndani ya mwili wako.

Ikimbie zinaa ya namna yoyote ile. Usimruhusu kijana wa kiume au wa kike akuzoee na kuvuka mipaka. Angalia unaongea naye nini huyo kijana. Unapotolewa pepo la uzinzi na halafu wewe mwenyewe ukaenda kuzini tena kwa kuzifuata tamaa za mwili wako fahamu anaweza kuutumia mlango wa dhambi hiyo hiyo kukurudia.

Usifanye punyeto au kujisaga, ukifanya hivyo baada ya kutolewa pepo la uzinzi fahamu huo unaweza kuwa mlango wa roho ya uzinzi kurudia tena.

ACHA UONGO, Biblia inasema shetani ni baba wa uongo. “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.” (Yohana 8:44).

Ukiipitia hiyo mistari utagundua dhambi ya uongo chanzo chake ni ibilisi mwenyewe, na mtu asemapo uongo huungana kabisa na mwanzilishi wa hiyo tabia. Yaani baba wa uongo ni shetani sasa angalia kitu hiki unaposema uongo unaungana kabisa na taasisi ya mwanzilishi wa uongo.

Ngoja nikuonyeshe kitu. Mungu aliumba miili yetu hii akaweka tendo la ndoa. Akaliweka litumike kihalali kwa wanandoa. Fahamu ni tendo lililoumbwa na Mungu shetani yeye anapowashawishi watu walifanye tendo lile lile kwa waisooana tunaita uzinzi.

Sasa kwenye uongo fahamu Mungu hajawahi kuumba hilo jambo. Linapofanywa na mtu fahamu halijachakachuliwa kama vile uzinzi. Yaani tendo la ndoa tuliumbiwa lakini kwa utaratibu uliowekwa. Adui anachofanya ni kukutoa tu kwenye utaratibu.

Uongo haukutoi kwenye utaratibu, unaungana na alichokizalisha yeye mwenyewe. Umenielewa lakini hapo? Unapojifunza somo la dhambi usifikiri dhambi zinafanana. Kuna zingine nguvu yake ni tofauti na nyingine.

Bahati mbaya sana watu wengi wanapoutazama uongo wanautazama kama ni dhambi ndogo sana. Aisee uongo ni dhambi mbaya sana sana. Mimi zamani zile kabla ya kuokoka nilikuwa mwongo sana, yaani nilizoelea na niliona uongo ni kitu cha kawaida tu. Niliupenda na niliusema kweli.

Yaani kusema uongo niliona ni kama umjini hivi. Nilipookoka Mungu akaanza taratibu kunifundisha tabia hii inavyomwudhi na asili yake ni wapi na waongo na shetani wakoje. Niliogopa sana. Kitendo cha kuiogopa hiyo dhambi ndiko kulifanya nianze kuichukia hii hiyo tabia.

Nilipoichukia tu nikashangaa ninaanza kuishinda taratibu mpaka leo hii mimi eti nawashangaa waongo na kujiuliza kwa nini huyu anasema uongo?

Uongo ni dhambi ambayo wapendwa wengi hasa Watanzania wanaipenda sana. Watu wengi hawapendi mtu anayewaambia ukweli. Wanapenda kuambiwa uongo mnaita “udaku”.

Yaani mtu analeta habari ina kaukweli asilimia tano lakini asilimia tisini na tano ni uongo mtupu. Hooo! huyo atauza sana habari yake. Watu si ndiyo wanapenda?

Hata kiongozi akiwa mkweli watu hawampendi, ngoja nikuchekeshe. Siku moja zamani zile nimetoka kuokoka alikuja mwalimu mmoja nampenda sana, alituuliza swali hivi leo mmeoga? Mmeogea sabuni gani? Akasema hivi kweli mtu umeokoka unaogea sabuni ya kufulia nguo?

Humo ndani asilimia tisini hivi tulikuwa tunaogea sabuni za kufulia. Yaani kipindi hicho mpendwa ni mtu aliyejizira hivi, mtu mchafu mchafu hivi eti ndiyo wa kiroho. Nakumbuka kipindi kile kulikuwa na vitambaa fulani vina urembo wa shangashanga yaani vilichomwa moto.

Mwalimu alipofundisha tena alichomekea kidogo tu habari za kuogea sabuni ya kufulia. Watu wengi walimchukia. Naamini wengi hata somo lile lote zuri alilolifundisha mwalimu yule hawakulishika. Unajua mimi nilitulia. Nikampenda yule mwalimu niliona yule katuambia ukweli kabisaaa.

Nikishangaa akija mtu akisema uongo hooo Mungu anataka tuogee foma. Foma ilikuwa sabuni ya kufulia ilikuwa ya unga sina uhakika kama miaka hii ipo. Watu ndiyo wanafurahi. Ohoo Mungu kasema watu waache kazi, tudumu kuhubiri na kuomba tuu!!! Watu ndiyo wanafurahia, mwalimu aliyesema kweli kuwa Mungu kasema asiyefanya kazi asile, watu wanamchukia.

Nilikaa chini nikagundua mkweli hapendwi tena haeleweki haraka. Nikaanza kuyachukia mafundisho ya uongo uongo yanayokuja kama yana ukweli hivi. Na nikagundua shetani ndiye chanzo cha hayo mafundisho ya uongo.

Sasa sirahisi kukubali ukweli, kwa sababu kuna vita kali mnooo kati ya ukweli na uongo. Bahati mbaya watu wengi mno wanapenda sana uongo kwa sababu hawajui madhara yake.

Wewe angalia watu kwenye vikundi vya maombi, kwaya nk. Utagundua dhambi hii imewabana wengi mnoo na inawaharibia kweli ila hawajui. Fikiria wewe ni mtumishi halafu unawaambia watu uongo, Ohooo! Mungu kanibariki sana mimi nina hiki na hiki. Hao watu siku wakigundua huna hivyo ulivyowaambia unavyo watakudharau sana.
Kwa nini usiseme ukweli tu? Fikiria unawaomba watu fedha au wakutunze kwa kusema uongo!!! Hooo! Mungu kaniambia fulani na fulani watoe kiasi fulani na tukanunue mabati. Kumbe Mungu hajakuambia ni uongo tu umeutunga.

Hivi ukisema ukweli tu kuwa ndugu zangu NAOMBA FEDHA NIKANUNUE MABATI BADALA YA KUMSINGIZIA MUNGU KUWA KASEMA?

Si useme tu MWENZENU SINA CHAKULA NAOMBA MSAADA!!! Nenda kwenye timu za maombi fuatilia maono yao usishangae kuona mtu anatengeneza ono kiuongo-uongo kabisaa kisa akubalike aonekane kuwa na yeye Mungu anamuonyesha.

Sikiliza mpendwa dhambi hii ni mbaya mnooo tusiiendekeze kabisa tuikatae. Fikiria mtu anamsemea maneno ya uongo kwa watu, mke wake au mume wake huku akishinda kanisani hashituki hata kushituka?

Umewahi fikiria makuhani na waandishi walimshitaki Bwana Yesu Kristo kwa uongo tu?  Yohana aliwaambia hawa watu maneno haya. “Askari nao wakamwuliza, wakisema, Sisi nasi tufanye nini? Akawaambia, Msidhulumu mtu, wala msishitaki kwa uongo; tena mtoshewe na mshahara wenu.” (Luka 3:14)

Umewahi fikiria leo hii watoto wa Mungu wanavyoshitakiana tena mashitaka ya uongo? Ukiingia ndani ya uongo utagundua humo ndani kufungwa, wivu, husuda, mashindano, kiburi, uuaji, majivuno, hasira, ukatili, chuki, nk.

Huwezi kumsemea mtu umpendaye uongo, huwezi kumsemea uongo mtu usiyeshindana naye nk. Uongo ni dhambi mbaya mnoo kuliko unavyofikiria.

Tena ni dhambi inayowaambukiza na kuwaangamiza wengine. Ngoja nikupe mfano. Nikikuambia uongo na ukaniamini na wewe utaenda kumwambia mwingine uongo na yeye akikuamini maana yake woooote mliouamini uongo mnangia kwenye kapu moja la WAONGO.

Umewahi kufikiria hili? Ukidanganya na watu wakadanganyika fahamu wote wanaingia kwenye kundi la wadanganyifu. Sasa angalia ulivyomtumikia shetani kwa neno la uongo tu? Ukawaingiza wooote kwenye dhambi hiyo.

Dhambi hii ina sehemu kubwa sana ya kuyafanya mapepo yawarudie watu walioondolewa mapepo ambao hawajauacha uongo.

Unajua dhambi ya uongo na uzinzi vipo jirani mno ni kama pua na mdomo hivi. Wewe wafuatilie waongo wengi, utagundua wengi ni wazinzi. Fuatilia mwanamke mzinzi hawagi mkweli. Mfuatilie mwanaume mzinzi utagundua ni mwongo kweli kadanganya wasichana wengi mnoo, mwanamke mzinzi ni vivyo hivyo anawadanya wanaume wengi kweli mnoo.
Kwa hiyo jihadhari mno na dhambi hii kama umeombewa na mapepo yakatoka ili yasikurudie acha uongo. Umenielewa? Acha hiyo tabia ni dhambi mbaya. Sema ukweli upende ukweli uwe vile ulivyo usimdanganye mtu kwa kuishi kwa kuigiza.

Jambo lingine ni hili JIFUNZE KUZIHIFADHI NGUVU ZA MUNGU KWA WINGI NDANI YAKO.
Msikilize Bwana Yesu Kristo asemavyo.

“Lakini, ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia.Mtu mwenye nguvu aliyejifunga silaha zake, alindapo nyumba yake, vitu vyake vi salama;lakini mtu mwenye nguvu kuliko yeye atakapomwendea na kumshinda, amnyang’anya silaha zake zote alizokuwa akizitegemea, na kuyagawanya mateka yake. Mtu ambaye si pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutawanya. Pepo mchafu amtokapo mtu, hupitia mahali pasipo maji, akitafuta mahali pa kupumzika; asipoona, husema, Nitairudia nyumba yangu niliyotoka. Hata afikapo, akaiona imefagiwa na kupambwa, ndipo huenda akachukua pepo wengine saba, walio waovu kuliko yeye mwenyewe, wakaingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza.” (Luka 11:20:26)

Ukiipitia hiyo mistari utagundua pia ili mtu asiingiliwe na adui ni lazima awe na nguvu na silaha.

Ngoja nijaribu kukuonyesha kwa ufupi. Ili leo ndani yako uwe na nguvu za Mungu, ni lazima umruhusu huyo Mungu mwenye hizo nguvu akae ndani yako. Huwezi kumtofautisha Mungu na Bwana Yesu Kristo na Roho Mtakatifu. Kwa hiyo ili nyumba yako au mwili wako uweze kupewa nguvu za Mungu ni lazima uhakikishe unampokea Bwana Yesu Kristo moyoni au ndani yako.

Ni hatari sana ukalitoa pepo ndani ya mtu na mtu huyo ndani yake asiwe na mtoaji pepo yaani Roho Mtakatifu. Maandiko yanasema hivi. “Lakini mimi nikitoa pepo kwa Roho wa Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia.” (Mathayo 12:28)

Umeona pepo anatolewa kwa Roho Mtakatifu. Kwa lugha nzuri mapepo kiboko yao ni huyu Roho Mtakatifu. Sasa unapomhifadhi huyu Roho Mtakatifu ndani yako ni ngumu mno kwa pepo kukufuatilia.

Fanya hivi. Hakikisha kila siku unasoma neno la Mungu. Kumbuka neno la Mungu ni moto au ni nguvu au upanga wa Roho wa Mungu. Soma neno liweke moyoni mwako lifanyie kazi. Jifunze kusikiliza mafundisho au mahubiri ya neno la Mungu.

Hakikisha kila siku uwe na muda kuomba wewe binafsi. Omba Ulinzi wa Mungu kwako, ombea na watu wengine. Omba ujazo wa Roho Mtakatifu na nguvu zake zijae ndani yako.

Usiache kwenda kanisani au kwenye vikundi mbalimbali vya maombi au mahali neno la kweli linasema hapo. Ni rahisi kuwa na nguvu za Mungu ukifanya hayo niliyokuambia.
Naamini umenielewa katika hili somo lote nililokuahidi kukufundisha.

Mungu akubariki sana.

Ukihitaji masomo yetu unaweza kuyapata kwa njia hizi zifuatazo:-

1. App yetu ya huduma yenye jina  “MWAKATWILA” utaipata kwenye link hii 👉🏼https://goo.gl/rSzZfJ

2. Tovuti yetu ya www.mwakatwila.org

3. YouTube - Mwakatwila au HUDUMA YA SOMA NENO LA MUNGU (HUSONEMU).

4. Facebook ingia katika hiyo tovuti au website yetu utaona alama ya Facebook(f) like na utapata maelezo ya kujiunga au ingia Facebook halafu andika  “SOMA NENO LA MUNGU”

5. Instagram ingia Instagram app halafu andika “Steven Mwakatwila”

6. DVDs 📀 au CDs 💿

7. VITABU.
NB: Wasiliana na mhudumu ofisini kwa namba +255 763 109 733, kupata VITABU, DVD & CD.

8. Kwa njia ya REDIO:- Utapata mafundisho yetu kwa redio zifuatazo:-
➖Rungwe FM 102.5 Kila siku ya Jumapili  saa tatu mpaka saa nne usiku.
➖Baraka FM 107.7 Kila siku ya Jumanne saa kumi na mbili jioni mpaka saa moja usiku.
➖Bomba FM 104.1 Kila siku ya Ijumaa saa tatu usiku mpaka saa nne usiku.

9. Unaweza kutupata kwenye ONLINE RADIO yetu:-  radio.mwakatwila.org

Kwa Mawasiliano zaidi Utatupata kwa namba hizi:-
+255 754 849 924 Au +255 756 715 222

Wako
Mwl Steven & Beth Mwakatwila.
01/04/2019

Thursday, March 28, 2019

2⃣4⃣ MAMBO MUHIMU UNAYOTAKIWA UYAFANYE ILI UPATE KUISHINDA DHAMBI YA UZINZI

Na: MWL STEVEN & BETH MWAKATWILA

FUATANA NASI:- KWENYE APP, FACEBOOK, INSTAGRAM, ONLINE RADIO 📻, WHATSAPP, WEBSITE & YOUTUBE, Kwa links zilizoko kwenye HII LINK hapa:

KUPATA APP YETU “HUSONEMU (MWAKATWILA) APP” BONYEZA LINK HII HAPA:

🗓 28 Machi, 2019

Bwana Yesu Kristo asifiwe sana. Naamini unaendelea vizuri. Nimekuletea mfululizo wa somo nililokuahidi kukufundisha. Kumbuka katika kipindi kilichopita  nilikuonyesha eneo lile la namna ya kufanya ikiwa utaona dalili za kuwa kuna pepo la uzinzi  ndani ya mwili wako.

Nilikufundisha kuwa jambo la kufanya ni kulitoa tu hulo pepo.

Ngoja tuendelee mbele kidogo pepo hatakiwi atulizwe, anatakiwa atolewe ndani ya mtu. Na pia asipewe nafasi ya kumrudia huyo mtu tena.

Bwana Yesu Kristo siku moja alikutana na mtu mwenye pepo angalia alipokuwa analitoa alilipa amri ya kutokumrudia huyo mtu tena. “Naye Yesu akiona ya kuwa mkutano unakusanyika mbio, akamkemea yule pepo mchafu, akamwambia, Ewe pepo bubu na kiziwi, mimi nakuamuru, mtoke huyu, wala usimwingie tena. Akalia, akamtia kifafa sana, akamtoka; naye akawa kama amekufa; hata wengi wakasema, Amekufa. Lakini Yesu akamshika mkono akamwinua naye akasimama.” (Marko 9:25-27).

Ukiipitia hiyo mistari utaona wazi kuwa Bwana Yesu Kristo alitoa amri ya huyo pepo asimrudie huyo mtu tena. Unapoisoma hiyo mistari unaona umuhimu wa sisi leo tunapoyatoa hayo mapepo yaliyo ndani ya watu tujifunze kutoa amri kwa hayo mapepo kutowarudia hao watu tena.

Kumbuka huduma hii inabebwa na mamlaka ya ufalme wa Mungu. Kwa hiyo kinachoamrishwa kitatii kile kilichosemwa na mtoa amri kwa sababu amebeba mamlaka.

Mara nyingi tunajisahau sana tunapoyatoa hayo mapepo ndani ya watu kuyawekea amri hii ya kutokuwarudia hao watu tena. Unajua ulimwengu wa roho unaheshimu mno kile kilichosemwa kimamlaka. Pepo hatoki kwa kupenda anaamriwa na pia lazima aamriwe asirudi hapo alipotolewa.

Unaposoma maandiko unaona sababu nyingi tu zinazopelekea mtu kurudiwa na pepo.
Sababu nyingine ambayo inaweza kumfanya pepo wa uzinzi arudi kwa mtu aliyetolewa pepo ni HOFU KWA HUYO MTU ALIYETOLEWA PEPO.

Watu wengi waliotolewa pepo huwa wamebeba hofu ya kuona watarudiwa na hali hiyo tena. Maandiko yanasema kile unachokihofu ni rahisi sana kukupata. “Aogopacho mtu asiye haki ndicho kitakachomjilia; Na wenye haki watapewa matakwa yao.” (Mithali 10:24).

Unapotolewa pepo hilo jenga ndani yako imani isiyo na hofu kuwa litakurudia hata ukiona dalili za kuwaka tamaa ya uzinzi. Kumbuka mwili unaweza kuwasha tamaa ya kufanya tendo la ndoa.

Sasa wengi wanapokutana na hali hii ya mwili kuwaka tamaa badala ya kuushughulikia mwili huanza kufikiria ile hali yao ya kwanza ya pepo la uzinzi imewarudia.
Hubeba hofu na hofu hiyo huwaharibu katika imani na mwisho kweli huyo pepo huwarudia. Ukifanyiwa huduma ya namna hii jenga imani usiwe na mashaka kuwa halijatoka, au litarudi hata uonapo dalili yoyote.

Shetani ni mjaribu na mwongo, atakujaribu tu na kukudanganya kwa kukutisha kwa kukuonyesha kuwa hajatoka. Akiona imani uliyonayo kuwa huna pepo hilo tena atakuacha.

Unajua mtu mwenye hofu au mashaka maana yake hajaamini. Nenda kaombewe ukiambiwa na waombaji hao kuwa pepo ametoka amini. Ukiambiwa bado hajatoka usisite kuendelea kuombewa mpaka upate uhakika kuwa ametoka.

Ukiambiwa ametoka jenga imani hapo usihofu kuwa hajatoka hata kama alisumbua sana kutoka.

Sababu nyingine ni DHAMBI.
Nataka nikutazamishe hapo dhambi kwa aina mbili, kuna dhambi ikiyotangulia kufanywa na dhambi aifanyayo mtu huyo baada ya kutolewa pepo.
Nianze kwa dhambi iliyotangulia kufanywa. Kuna watu ambao wamejikuta wakiwa na mapepo kwa sababu ya kuyafungulia mlango wao wenyewe  kwa viapo au maangano fulani.

Wanaweza wakawa ni wao wenyewe au waliowatangulia, watu wa namna hiyo hujikuta wamefungiwa au kubanwa na hayo mapepo kihalali.

Biblia inasema hivi “Je! Aliye hodari aweza kunyang’anywa mateka yake, au jeshi lao waliofungwa halali wataokoka?” (Isaya 49:24).

Umeona hapo? Kuna wafungwa waliofungwa kihalali kabisaa, kwenye ulimwengu wa roho kuna watu wamefungwa na vifungo mbalimbali kihalali. Maana yake kuna makosa yalifanyika au maagano fulani yalifanyika na hayo ndiyo yanayotumika kumpa shetani na mapepo uhalali wa kuwabana au kuwafungia watu hata tabia mbaya zilizobebwa na mapepo.

Sasa unaweza kuombewa pepo akatoka lakini akarudi haraka kwa sababu bado ana uhalali wa kumtesa huyo mtu kwa sababu ya kutokutubiwa au kuondolewa kitu kile  kinachompa uhalali huyo pepo wa kumfuatilia huyo mtu.

Ngoja nikupe mfano huu. Kuna ndugu alikuwa amewekewa ndani ya tumbo lake hirizi. Aliwekewa na mganga kwa kutumia maji aliyoyaoga tu. Mganga huyo akamwambia nimekuwekea zindiko tumboni.

Sasa siku mimi nakutana naye anaumwa ili nimwombee pepo akalipuka. Ilinichukua zaidi ya masaa nane kumwombea ili hilo pepo limwachie mpaka alipokunya hiyo hirizi.
Alipoitoa hiyo hili kwa kupitia njia ya haja kubwa tu akafunguka. Uhalali wa hilo pepo kumbana na kumfuatilia huyo mtu ulikuwa katika ile hirizi aliyokuwa nanyo ndani ya tumbo lake.

Unajua siku ile nilijifunza kitu kikubwa sana. Kuna watu walipewa vitu na wachawi au waganga wa kienyeji vinaonekana vya kawaida tu kumbe ndani yake vimebeba mapepo mengi tu. Sasa unaweza kukemea hilo pepo litoke, pepo litatoka lakini kama kile alichopewa huyo mtu hakijashughulikiwa fahamu pepo anapata uhalali wa kurudi hapo kwa sababu kibebeo chake kikichombeba huyo pepo na kumwingia huyo mtu bado kipo

Cha msingi hapo wewe mwenye hiyo shida yaani hilo pepo usisite kumweleza ukweli huyo mtumishi chanzo cha wewe kuingiliwa na hiyo roho. Watu wengi hujitahidi sana kuficha mambo yao mabaya. Hilo linawagharimu sana.

Unakuta mtu anakueleza leo kimoja ndani ya vitu kumi ambavyo ilitakiwa akueleze. Watumishi wengi wakikuona siyo mkweli au haupo wazi kwao wanakuacha. Wakifikiri wewe hupendi kufunguliwa.

Eleza ukweli, mwingine anasema kwani Mungu hawezi kumuambia huyo mtumishi? Si kila mtumishi ni nabii. Nabii anaona anasikia kwa uwazi mno mambo ya ulimwengu wa roho. Na si kila kitu nabii pia huonyeshwa. Huyo nabii pia ni mtu anaweza ona na kusikia asielewe kabisaa.

Sasa fikiria wewe unayejua ukweli hauusemi unaficha. Unapokuwa mkweli fahamu ndipo unapowekwa huru mapema mnoo. Unapomueleza mtumishi dhambi yako au yenu iliyofungulia mlango wa pepo kuwafuatilia ni rahisi kufanya toba iliyonyooka.

Mnapofanya toba na kuachilia damu ya Yesu Kristo mahali palipokosewa ili iondoe hiyo dhambi ndipo uhalali wa hayo mapepo kukumiliki unapokosa nguvu  na yanapotolewa ni ngumu kuludi kwasababu hayana haki tena ya kukumiliki.

Ndiyo maana mkianza kufanya maombi ya toba tu utaona  mapepo yanaanza kupata shida mno mahali hapo. Nimeona mara nyingi tu. Mnapokuwa katika kusanyiko lenye watu wengi, mnapoanza kufanya maombi ya namna hiyo tu, usishangae kuona mapepo yanaanza kuangaika.

Mengine yatapiga kelele mengine kuanguka chini  yatafanya kila aina ya fujo. Toba ya kweli inamwondolea shetani uhalali wa kuwamiliki watu. Dhambi ndiyo chanzo kikubwa cha kumpa adui uhalali wa kummiliki mtu na kumtesa.

Naamini umenielewa. Angalia je! Kuna uhalali wowote umpao shetani kukumiliki? Tubia hapo. Mweleze huyo mtu anayekuombea nini unaona kinampa adui nafasi ya kukumiliki. Ndiyo itakuwa rahisi pepo kutoka au kutokukurudia.

Mungu akubariki sana

Wako

Mwl Steven & Beth Mwakatwila


  • 28-03-2019

Saturday, March 23, 2019

2⃣3⃣ MAMBO MUHIMU UNAYOTAKIWA UYAFANYE ILI UPATE KUISHINDA DHAMBI YA UZINZI

2⃣3⃣ MAMBO MUHIMU UNAYOTAKIWA UYAFANYE ILI UPATE KUISHINDA DHAMBI YA UZINZI

Na: MWL STEVEN & BETH MWAKATWILA

FUATANA NASI FACEBOOK

FUATANA NASI INSTAGRAM

KUPATA APP YETU “HUSONEMU (MWAKATWILA) APP”, BONYEZA LINK HAPA:

FUATANA NASI WHATSAPP

FUATANA NASI YOUTUBE
&
FUATANA NASI ONLINE RADIO

🗓 23 Machi, 2019

Bwana Yesu Kristo asifiwe. Nianze kwa kukuomba msamaha kwa sababu ni muda mrefu kidogo sikukuletea mfululizo wa somo hili.

Nimekuwa na mambo mengi kweli kweli sasa kuupata muda wa kukuandikia somo ndiyo inakuwa taabu kidogo. Nimeupata huu muda nimeona niiutumie kukuandikia na  kukuletea somo hili.

Katika kipindi kilichopita nilikuwa nakuonyesha  mlango wa pili wa tabia ya uzinzi nayo ilikuwa ni pepo au roho ya uzinzi.

Hebu tusogee mbele kidogo nataka kukuonyesha namna ya kufanya ili utoke kwenye tabia ya uzinzi iliyotokana na pepo.

NJIA YA KWANZA NI; KUTUMIA MAMLAKA MAALUMU YA KULITOA HILO PEPO MWILINI MWAKO.

Ikiwa unaona dalili zote za kuwa una roho au pepo la uzinzi mwilini mwako na unataka uondokane na hiyo tabia ya uzinzi njia ya kutoka hapo ni kulitoa hilo pepo mwilini mwako.

Fahamu pepo hilo ndilo linalozalisha hiyo tabia na ili hiyo tabia iondoke ni lazima ulitoe hilo pepo ndipo hiyo tabia utaicha.

Unaweza ukawa umeokoka kabisa lakini hiyo roho ukawa nayo kabisa. Wengi huhisi kama hawajaokoka vizuri. Sikiliza kuokoka ndiyo hatua ya kwanza ya kukamilishwa.
Unapookoka ndipo unaanza kutengenezwa mpaka kufikia utimilifu. Kwa maana hiyo unaweza kuokoka au kuupokea wokovu lakini ukawa bado na pepo tu.  

Mpaka utakapoanza kufundishwa na kukutana na watu waliotangulia katika huo wokovu waitwao watumishi  ambao watatumia mamlaka waliyopewa na Mungu ya kuwakamilisha hao waliookoka.

Na moja ya ukamilishaji wao ni huu wa kuyatoa hayo mapepo yaliyo ndani ya hao waaminio. Biblia inatufundisha hivi “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe;” (Waefeso 4:11-12)

Mungu anajua kuwa watakatifu au watu waliotengwa kwa ajili yake au waliochaguliwa si wakamilifu na wanahitaji kukamilishwa. Sasa angalia watu wengi wanaingia ndani ya wokovu wakiwa na tabia mbaya tu zingine zimebebwa kwenye mwili zingine zimewabana kwa kutumia roho au mapepo.

Kuongozwa sala ya toba au kubatizwa usifikirie kunaweza kuondoa pepo. Hili ni jambo muhimu sana ambalo unahitaji ulijue. Unaweza batizwa na pia kuongozwa sala ya toba lakini bado ukawa na pepo la uzinzi tu.

Pepo litamuachia mtu atakayefanyiwa huduma maalumu ya kulitoa hilo pepo kwa njia ya kuliamuru limtoke huyo mtu kwa kutumia jina la Bwana Yesu Kristo.

Bwana Yesu Kristo anatufundisha hivi. “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya;” (Marko 16:17).’

Pepo anatolewa. Kama hakujafanyika kazi hiyo ya kumtoa hapo alipo fahamu atakuwepo tu, mpaka watu wajue kuwa kuna pepo au wafanye huduma maalumu ya kuyaamuru mapepo yaliyo ndani ya watu yawatoke ndipo unaweza ukashangaa hata watu ambao hukuwahi fikiria wana mapepo siku hiyo ukagundua kuwa walikuwa na mapepo.

Nakumbuka mwaka fulani nilisukumwa kufanya huduma maalumu ya namna hii kwa ajili ya wanakamati unajua kilichotokea? Mapepo yalilipuka kwa watu ambao hata sikuwafikiria.

Siyo kuwa hawajaokoka na hawampendi Bwana Yesu Kristo, mapepo yanaweza kabisa yakaja hata mahali watoto wa Mungu wamekusanyika. Unaweza kuniuliza kivipi.

Angalia mistari hii uone. “Ilikuwa, siku moja ambayo hao wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha mbele za BWANA, Shetani naye akaenda kati yao.BWANA akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu BWANA, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha BWANA akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.Ndipo Shetani akamjibu BWANA, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha BWANA bure?” (Ayubu 1:6-9)

Ukiipitia hiyo mistari ndipo utanielewa vizuri au utaelewa kwa nini neno la Mungu linasema mpingeni shetani. Angalia hii mistari. “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili.” (Yakobo 4:7-8)

Maandiko yanatufundisha kuwa watoto wa Mungu walipojihudhurisha mbele za Mungu shetani na yeye akaenda kati yao. Maana yake miongoni mwao kuna mtu ndani yake alimbeba  shetani kabisa. Unanielewa lakini?

Ngoja nijaribu tena kukuonyesha hili jambo. Maandiko yanasema mpingeni shetani naye atawakimbia mkaribieni Mungu naye atawakaribia. Fikiria kidogo hao wanaoambiwa wampinge ni watoto wa Mungu kabisa, kabla hawajamkaribia Mungu wanatakiwa wampinge kwanza shetani inamaana wale wana katika kipindi kile cha Ayubu hawakushughulikia jambo hilo walipomkaribia Mungu adui akawa kati yao.

Unajua hata kipindi kile cha Bwana Yesu yupo na timu yake ile shetani alijihudhurisha katikati yao kabisaa. Alikuwa ndani ya Yuda. Maandiko yanasema hivi. “Yesu akawajibu, Je! Mimi sikuwachagua ninyi Thenashara, na mmoja wenu ni shetani? Alimnena Yuda, mwana wa Simoni Iskariote; maana huyo ndiye atakayemsaliti; naye ni mmojawapo wa wale Thenashara.” (Yohana 6:70-71).

Bwana Yesu Kristo alilijua jambo hili kabisa kuwa katika ile timu yake shetani yupo lakini hakumpinga au kumtoa. Na kweli alikuja kumsaliti. Angalia kitu hiki labda utaelewa kuwa mapepo yanaweza kumwingia mtu aliyeokoka kabisaa angalia mfano huu.

“Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni. Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda. Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni. Ndipo alipowakataza sana wanafunzi wake wasimwambie mtu ye yote ya kwamba yeye ndiye Kristo Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema, Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.” (Mathayo 16:17-23).

Ukiipitia hiyo mistari utagundua Bwana Yesu Kristo alilitoa pepo au shetani aliyekuwa ndani ya Petro. Petro alishakuwa amepewa taarifa kuwa atapewa ufunguo au mamlaka kubwa sana katika ufalme wa Mungu. Petro huyo huyo shetani alimwingia.

Hebu jiulize swali Bwana Yesu alikuwepo shetani akamwingia Petro je! Asingefanya huduma ya kumtoa huyo shetani Je? Petro angeondolewa huyo shetani kisa eti ni mtumishi au ameokoka? Bwana Yesu Kristo hakumkemea  shetani au pepo aliyekuwa ndani ya Yuda kwa sababu alikuwa anataka kutimiza maandiko katika habari za kusalitiwa kwake.

Naamini kama isingekuwa hivyo angemkemea au kumtoa shetani ndani ya Yuda. Naamini umenielewa sasa ninavyokuambia kuwa tatizo kubwa ambalo watu wengi wanalo ni hili la kutokufanyiwa maombi mara kwa mara ya kuondolewa mapepo yaliyo ndani yao.
Biblia inatufundisha kuwa moja ya kazi ambayo Bwana Yesu Kristo alikuwa akiifanya ni kuyatoa mapepo yaliyo ndani ya watu.

Angalia mistari hii. “Hata kulipokuwa jioni, wakamletea wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa neno lake, akawaponya wote waliokuwa hawawezi, ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu.” (Mathayo 8:16-17)

Angalia na mistari hii  “na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba,” (Luka 8:2)

Ukiipitia hiyo mistari utagundua kuwa moja ya kazi aliyokuwa anaifanya Bwana Yesu Kristo ni hii ya kukemea au kuyaondoa mapepo yaliyo ndani ya miili ya watu.  Kazi hii hata leo hii Bwana Yesu Kristo anataka kuona ikiendelea kufanywa. Ndiyo maana anasema hivi. “Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina.” (Mathayo 10:1)

Maandiko yanasema waliopewa wajibu wa kuyatoa hayo mapepo ni wanafunzi. Unaposoma neno wanafunzi lina utofauti sana na ukisoma neno mitume. Unaweza ukawa mwanafunzi lakini usiwe mtume. Watu wengi hawajui kuwa unapofanyika kuwa mwanafunzi tu wa Bwana Yesu Kristo kwa kumpokea na kumwamini kama Bwana kwako unapewa hii nafasi ya kuyatoa mapepo yaliyo ndani ya watu.

Tatizo tulilonalo ni mfumo uliopo ndani ya kanisa. Wanafunzi wa Bwana Yesu hawaandaliwi hawakufundishwa mambo kama haya. Biblia inasema “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.” (Mathayo 28:19-20).

Moja ya jambo Bwana Yesu Kristo katuamuru tulifanye ni hili la kuyatoa mapepo. Sasa angalia kama wanafunzi leo hii wamefundishwa jambo hili. Ndiyo maana utaona wanafunzi wengi wa Bwana Yesu Kristo na watu wengine wasio wanafunzi wamebanwa na mapepo ya uzinzi.

Sikiliza mwanafunzi wa Bwana Yesu Kristo anapoona mwanafunzi mwenzake ana dalili za roho au pepo ndani yake ilitakiwa yeye ndiye alishughulikie hilo pepo. Sasa siku hizi mpaka akatafutwe mtume au nabii.

Amri ya kutoa pepo walipewa hata wanafunzi, siyo manabii au waalimu au wachungaji au wainjilisti au mitume tu. Wakifundishwa hao wanafunzi wakaamini kuwa wanayo hayo mamlaka nakuambia ukweli watayatoa mapepo mengi tu yaliyo ndani ya watu.

Ili kukabiliana na tabia ya uzinzi iliyoletwa na pepo lazima pepo hilo au mapepo hayo yatolewe ndani ya mtu huyo, kinyume cha hapo atakuwa mzinzi tu hata awe mwimbaji au mwombaji nk.

Ikiwa unaona dalili kama hizi tafuta wanafunzi wenzio wa Bwana Yesu Kristo au watumishi wenye ufahamu walitoe hilo pepo likitoka tu fahamu tabia ya uzinzi iliyoletwa na pepo itakuacha.

Mungu akusaidie na kukuongoza vema katika hatua hii. Katika somo lijalo nitakuonyesha sababu ya watu wengine kurudiwa na mapepo baada ya kutolewa ndani yao.

Ukihitaji masomo yetu unaweza kuyapata kwa njia hizi zifuatazo:-

1. Tovuti yetu ya www.mwakatwila.org

2. YouTube - Mwakatwila au HUDUMA YA SOMA NENO LA MUNGU (HUSONEMU).

3. Facebook ingia katika hiyo tovuti au website yetu utaona alama ya facebook(f) like na utapata maelezo ya kujiunga au ingia Facebook halafu andika  “SOMA NENO LA MUNGU”

4. Instagram ingia Instagram app halafu andika “Steven Mwakatwila”

5. DVDs 📀 au CDs 💿

6. VITABU.
NB: Wasiliana na Mhudumu ofisini kwa namba +255 (0) 763 109 733, kupata VITABU, DVD & CD.

7. Kwa njia ya REDIO:- Utapata mafundisho yetu kwa redio zifuatazo:-
➖Rungwe FM 102.5 Kila siku ya Jumapili  saa tatu mpaka saa nne usiku.
➖Baraka FM 107.7 Kila siku ya Jumanne saa kumi na mbili jioni mpaka saa moja usiku.
➖Bomba FM 104.1 Kila siku ya Ijumaa saa tatu usiku mpaka saa nne usiku.

8. Unaweza kutupata kwenye ONLINE RADIO yetu:-  radio.mwakatwila.org

Kwa Mawasiliano zaidi Utatupata kwa namba hizi:-
+255 (0) 754 849 924 Au +255 (0) 756 715 222

Wako
Mwl Steven & Beth Mwakatwila.
23/03/2019